Pages

Subscribe:

Wednesday, June 29, 2016

HADITHI: NYUMA YA MACHOZI (sehemu ya kumi) 10



MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
ILIPOISHIA:
“Jimmy, mzigo wako huu hapa, hizi ni laki na nusu, hamsini za kusafishia na laki moja adivansi ukileta picha zangu nakumalizia laki na nusu. Ila kuna zawadi yako kubwa kama utakuwa msiri, kuna kazi nyingine ya milioni moja.”
“Wacha!”
“Wewe tu kuonesha uaminifu.”
“Basi dada kesho saa nne nakuletea mzigo wako, andaa fedha yangu tu.”
“Hakuna tatizo, tutaonana kesho, lakini chonde chonde siri hii asijue mtu yeyote.”
“Nakuhakikishia siri hii itabakia kwa watu wawili mimi na wewe tu.”
“Haya, usiku mwema.” SASA ENDELEA...

Kilole aliagana na Jimmy na kurudi ndani, alipofika kitandani alivua nguo zote na kujilaza pembeni ya Kinape. Alfajiri kilevi kilipomwisha Kinape alishtuka...
usingizini, akili yake alijua aliyelala pembeni yake ni mpenzi wake Happy, lakini alipoangalia vizuri aligundua ni Kilole, alishtuka na kunyanyuka kitandani. Alishangaa kujikuta amelala kitanda kimoja na shemeji yake na kwa hali waliyokuwa kuwa nayo, aliamini lazima walifanya mapenzi. Alijiuliza ilikuwaje mpaka akawa kwenye kitanda cha rafiki yake wakiwa watupu na mkewe.

Alinyanyuka haraka kitandani na kupitia nguo zake bila kuzivaa na kukimbilia chumbani kwake. Alipokuwa akipapatika kama kuku aliyekatwa kichwa na kuachiwa, Kilole alikuwa akimuangalia kwa chati huku akichekea moyoni huku akisema:
“Kiko wapi, mimi na wewe nani mjanja.”
Hakujisumbua aliendelea kulala huku akichelelea moyoni, wakati huo Kinape baada ya kuingia chumbani kwake na kukaa kitandani mikono aliweka kichwani na kujiuliza kilichotokea ni kweli. 

Ili kupata ukweli alizishika sehemu zake za siri na kukutana na majimaji kumuonesha kabisa katumika. Kila alivyorudisha mawazo yake ilikuwaje mpaka akalala katika kitanda cha rafiki yake kipenzi Deus na mkewe, jibu lilikuwa mbali.
Alikumbuka siku ya jana yake kwenye sherehe baada ya kuondoka Happy alibakia na shemeji yake Kilole wakipiga stori huku wakivuta muda kumsubiri Happy ili wafungue sherehe rasmi.

Wazo lake la haraka lilikuwa huenda ule ulikuwa mpango wa Kilole kama alivyomuahidi atahakikisha anamrudisha mikononi mwake. Kinape alijiapia kuwa kamwe pamoja na kufanya ujanja ule hawezi kuendelea kuwa mpenzi wake zaidi ya kuhama nyumba. 

Wakati anatoka kuoga aliona simu yake juu ya kochi, aliichukua na kukuta imezimwa, alielekea nayo chumbani kwake. Alipoingia aliiwasha, haikupita muda ziliingia meseji zaidi ya kumi zote zikuwa za Happy akimlalamikia kwa kitendo alichomfanyia cha kumzimia simu.

Wakati akiendelea kusoma ujumbe wa Happy simu yake iliita, alikuwa Happy, alijiuliza atamwambia nini ili amuelewe. Lakini alijikaza kiume na kuipokea kwa kuamini hawezi kukosa cha kumueleza.
“Haloo Kinape umenifanya nini?”
“Happy mbona huniulizi nimepatwa na nini unaanza kunilaumu.”

“Kinape, nilikuambia narudi, lakini nilipofika nyumbani nikakuta hali ya mama ipo sawa, nimerudi nikasikia umenifuata na kusema utarudi kesho.
Nilipopiga simu yako kumbe uliiacha ndani kwa kuchanganyikiwa. Kinape, tulikuwa na mpango gani wa kulala pamoja na kusababisha sherehe ya shemeji yako kuvurugika?” Maneno yale yalimpa picha na kujua atamjibu nini ili kumfanya asiendelee kuumia.
“Mpenzi nilipokuwa nakuja kwenu, nilipata na ajali na kupelekwa polisi hata simu niliisahau nyumbani.”
“Sasa mbona baadaye nilipokutafuta ilikuwa imezimwa?”
“Nilikuta haina chaji.”

“Kwani ulirudi saa ngapi?”
”Saa nane usiku.”
“Ooh, pole upo wapi sasa?”
“Nyumbani.”
“Nakuja sasa hivi?” “Usije nisubiri kwenu.”
“Hapana mpenzi usisumbuke nakusubiri nitakufuata hapo hapo.”
“Sipo nyumbani, ndiyo maana nimekueleza nisubiri.”
“Kinape si umeniambia upo nyumbani sasa hivi! Mbona sikuelewi?”
“Nimetoka nyumbani sasa hivi kuelekea polisi, hivyo namalizana nao nipitie kwenu.”
“Mmh! Sawa.”
“Usisikitike dia, sawa.”
“Sawa dia, nimeumia sana kusikia umelala polisi kwa ajili yangu.”
“Hawakukupiga?”
“Hawakunipiga nipo sawa dia.”
“Ooh! Afadhari nakusubiri, una usafiri au nikufuate na gari?”
“Hapana, kuna teksi nilikodi,” Kinape alijitahidi kumzuia mpenzi wake.
“Hakuna tatizo mpenzi wangu, angalia usije ukapata ajali tena.”
“Unafikiri niligonga walaa, alijigonga mwenyewe mwendesha boda boda wala hakuumia polisi hawana dogo.”

“Mbona unaongea hivyo si upo polisi?”
“Nipo mbali nao.” “Basi kuwa makini nakupenda sana Kinape, mmmmmmwa.” “Mmmwa,” Kinape naye alijibu na kukata simu. Mara mlango uligongwa, alikuwa Kilole, bila kuitikia alinyanyuka na kwenda mlangoni, alipofungua alikutana naye uso kwa uso. “Za asubuhi shemeji?” Kilole alimsabahi Kinape aliyekuwa akimshangaa. “Nzuri.”
“Shemeji chai tayari.”
“Asante, nimeshiba.” “Imeanza lini na leo iwe ya pili, kama ulijua hunywi chai kwa nini hukuja kunieleza mapema. Si umenipita jikoni unakwenda bafuni kuoga.” “Sikukuona.”
“Basi lazima chai uinywe ndipo uende huko kwa mwanamke wako unayejifanya unampenda kuliko wanawake wote.”

“Shemu yote yamefikaje huko, tunazungumzia chai Happy kaingiaje?” Kinape alimuuliza Kilole huku akitengeneza shati lake. “Kama hutaki yote hayo, njoo unywe chai tena kuna kitu nataka unieleze kwa kituo kiniingie. Wewe si ulinikataa iweje univizie usiku?” Kilole alizungumza sauti ya kuonesha hakutendewa haki. “Mimi?” Kinape alishtuka kusikia vile. “Kwani hapa nazungumza na jiwe?” “Mmh! Bado sielewi nini kilitokea jana,” Kinape alisema akiwa ameangalia chini kwa aibu.
“Ndiyo maana nikasema kunywa chai tuzungumze.”
“Happy ananisubiri.”
“Happy wa muhimu kuliko tukio ulilonifanyia jana usiku, ulishindwa kuniambia nikakukubalia kwa hiyari yangu, ukanivizia nimelala huo si ubakaji? Nilijua bado unanipenda ndiyo maana nilikueleza nikupe penzi la siri kwa vile bado naheshimu penzi lako ukakataa. 

“Lakini asubuhi nashtuka nakuona unakimbia, kweli Kinape wewe wa kunifanyia hivyo?” Kilole alimuuliza kwa msisitizo.
“Kilole hili suala linatakiwa tulifanyie kazi si la kukurupuka kulaumiana.”
“Sijakulaumu ila nimekuuliza ulishindwa vipi kunieleza una hamu na mimi, siwezi kukunyima, kwa vile wewe ndiye uliyenionesha raha na tamu ya dunia. Hili kwangu si tatizo lakini na mimi nina ombi langu nakuomba nani unitekelezee ili tuwe sawa.”
“Mmh! Hata sielewi, basi niache niende kwa Happy ili nikirudi tupange vizuri.” “Kinape umenionjesha naomba unimalizie kabisa.”

“Sawa nimekubali, nikirudi nitatimiza haja zako.”
“Kinape kuna tatizo gani ukinipa muda huu ili ukitoka usiwe na wasiwasi wa kufikiria nyumbani?”
“Mmh! Sawa.”
Kauli ile ilimfanya Kilole amsukumie Kinape nyuma na kumuangushia kitandani kwake. Kama kipanga aliyeona kifaranga cha kuku alimsaula nguo zote na yeye kutoa zake chache zilizovaa.
Kinape alijikuta akiwa kama mbwa kwa chatu, moyoni alijiapiza atatafuta kila njia ahame pale ili kujiweka mbali naye. Upande wa Kilole aliamini mpango wake umekwenda vizuri tofauti na alivyofikiria na kuapa kumfanyia mambo makubwa Kinape. 

Baada ya kuondoka chumbani Kinape alibakia ameinama mikono kichwani alijiuliza maswali yasiyo na majibu, ilikuwaje akawa katika kitanda cha Deus, alichokumbuka kuamka asubuhi na kujikuta amelala na Kilole bila nguo bila kujua alifikaje pale.
Aliwaza labda ulikuwa mpango wa Kilole aliomuahidi hapo awali, lakini shutuma alizozitoa zilizidi kumchanganya kuonesha amemlazimisha kufanya naye mapenzi bila ridhaa yake. Kitendo kilicho onekana kuwa ni sawa na kubaka.
Japo hakupenda kufanya mapenzi tena na Kilole lakini kwa upande mwingine alimshukuru kwa uamuzi wake wa kutomshitaki polisi. Aliamini kama angempeleka basi angeweza kuozea gerezani, kwani ushahidi wote ulikuwepo wa kuonesha amebakwa. 

Simu yake iliita zaidi ya mara sita na kukatika, aliisikia lakini akili yake ilikuwa mbali sana. Alikumbuka alikuwa na mpango wa kuonana na Happy nyumbani kwao, alinyanyuka na kwenda bafuni kuoga.
Baada ya kumnaliza kuoga na kubadili nguo, alipoangalia simu yake alikuta aliyepiga ni Happy zaidi ya mara sita. Hakutaka kumpigia alijua yote atamalizia huko huko akifika, alitoka kuelekea nyumbani kwao Happy. Wakati anatoka sebule haikuwa na mtu alitoka haraka kumuwahi Happy, alipofika mlango wa kutokea nje aliitwa nyuma na Kilole.

 “Kinape.”
“Naam,” aliitika huku akisimama.
“Safari ya wapi?”
“Si nimekueleza nakwenda kwa Happy.”
“Nataka nikuambie kitu kimoja, sipendi kusikia jina la mwanamke wako, kila nikisikia linanitia kichefuchefu.”
“Lakini si mchumba wangu?” “Mmh! Sasa hii chai anywe nani?”
“Nilimuahidi nitakwenda kwao muda uliopita nikizidi kuchelewa atajisikia vibaya.”
“Kinape unachekesha, nisijisikie vibaya mimi niliyekutaka ukanikataa ukaishia kunibaka.”

“Yaani sijui hata ilikuwaje hiyo jana!”
“Iweje na wewe umeamua kunibaka.”
Kauli ile ilimmaliza nguvu Kinape na kubakia amesimama kimya kama amenaswa na sumaku.
“Kinape siwezi kukulazimisha mapenzi kwa vile upo na mchumba wako, lakini sipendi dharau.”
“Lakini si nimekueleza hali iliyopo?”
“Kinape huyo Happy angekujulia wapi kama mimi ningemgomea mume wangu wee kuja mjini?”

Kilole alimuuliza huku ameshika kiuno. “Lakini mbona yamekuwa hayo....,” Kinape alinyamaza kimya baada ya mlango kugongwa. Kilole aliamini muda ule Jimmy alikuwa akileta picha, alipofika mlangoni alikutana na Happy. Japo moyoni alichukia lakini alitengeneza tabasamu la uongo.”
“Ooh! Happy karibu.”
“Asante dada,” Happy alisema huku akimtaza Kinape aliyekuwa amesimama karibu na mlango. 

“Kinape unanifanya nini, nimekukosea nini mpaka uamue kunitesa hivi?” Happy alisema kwa sauti ya kilio.
“Happy mbona umekuwa mtu wa kulaumu bila kuuliza?”
“Niulize nini hapa ndiyo polisi?” “Hilo swali gani?”
“Kinape ni wazi hunipendi najipendekeza kwako,” Happy alilalamika huku machozi yakimtoka. “Happy unaniamini, huniamini?”

“Nikuamini vipi mtu muongo.” Wakati huo Jimmy mpiga picha alikuwa akiingia, ili kupoteza ushahidi Kilole alimueleza Kinape:
“Shemu naomba ukazungumzie nje mambo yenu nina mgeni.”
“Sawa,” Kinape aliitikia huku akimshika mkono Happy aliyekuwa ameiva na kuwa mwekundu kwa hasira.
“Hebu ngoja,” Happy alijitoa mkononi mwa Kinape. 

“Happy hebu msikilize mwenzako,” Kilole aliingilia kati baada ya kuona Happy akitafuta msaada kwake.
“Sikiliza dada, Kinape ananinyanyasa sana.”
“Mdogo wangu ngoja nizungumze na mgeni, tutalimaliza nina imani kabisa Kinape anakupenda sana.” Kinape na Happy walitoka nje na kuwaacha Kilole na Jimmy.
Itaendelea...

0 comments:

Post a Comment